VIBAKA WA KARIAKOO WAMUIBIA SIMU KOTEI, ALIKUWA AKINUNUA JUISI



Kiungo Mghana, James Kotei, juzi Jumatatu alikumbana na balaa la aina yake wakati akitokea mazoezini.

Akiwa maeneo ya Msimbazi alijikuta ikiingia mikononi mwa vibaka waliobobea kwa wizi na kumuibia simu ya mkononi yenye thamani ya Sh milioni 1.4, ambayo alipewa zawadi na mmoja wa wanachama wa Simba siku chache kabla ya mechi ya Ngao ya Jamii iliyoikutanisha Simba na Yanga kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar.

Habari zinaeleza, kuwa mara baada ya kufika makao mkuu wa klabu hiyo yaliyopo Mtaa wa Msimbazi alishuka katika basi la timu hiyo na kuanza kutembea kulekea katika Hoteli ya Sapphire anapoishi.

“Baada ya kutembea hatua chache hivi alipita sehemu kununua juisi ya miwa na hapo ndipo akajikuta akiibiwa simu hiyo.

“Simu hiyo alikuwa ameweka katika mfuko wa nyuma wa begi lake la mgongoni alilokuwa amebebea vifaa vyake vya mazoezi,” kilisema chanzo chetu cha habari.

Alipoulizwa Kotei kuhusiana na suala hilo alisema kuwa: “Ni kweli kabisa nimeibiwa simu jana (juzi), nilipokuwa nikitokea mazoezini, imeniuma sana kwani nimepoteza mawasiliano yangu mengi.

“Hata hivyo, imenibidi nitafute simu nyingine ambao natumia hivi sasa na namba yangu tayari nimeshairudisha ndiyo maana umeweza kunipata,” alisema Kotei.

SOURCE: CHAMPIONI

Maoni