AZAM FC KUCHEZA MECHI NNE ZA MAANA KATIKA KAMBI YA UGANDA

TIMU ya Azam FC ya Dar es Salaam, itacheza mechi nne za kujipima nguvu katika kambi yake ya Uganda kujiandaa na msimu mpya.
Hiyo inafuatia Vipers FC nayo kuthibitisha kucheza na mabingwa hao wa mwisho wa michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati Agosti 11, mwaka huu.
Mechi nyingine tatu za Azam FC Uganda ni dhidi ya KCCA Alhamisi ijayo saa 10.00 jioni, ikifuatiwa na hiyo wa Vipers, Ondurapaka Agosti 13 kabla ya kuhitimisha ziara kwa kukipiga na URA Agosti 14.
Azam FC iliyowasili nchini Uganda Jumapili, inatarajia kukaa kwa takribani siku 10 ikifanya maandalizi ya mwisho kuelekea msimu ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL).
Kocha Mkuu wa Azam FC, Aristica Cioaba, anaamini kikosi chake kitanufaika vilivyo kwa kuimarika na kuwa imara kwa msimu ujao kufuatia kambi hiyo ya siku 10 nchini humo.
Kikosi hicho kinatarajia kuendelea na programu yake ya mazoezi kwa siku ya pili leo jioni ili kujiweka sawa kabisa kabla ya mechi hizo na maandalizi kamili ya kuelekea msimu ujao.
Wakati huo huo, winga wa Azam FC Ramadhan Singano ‘Messi’, jana usiku aliungana na wachezaji wenzake kambini nchini humo akitokea Dar es Salaam.

Maoni