Chid tena kwenye madawa

Rapa Rashid Makwiro 'Chid Benz’ amekamatwa akiwa na wenzake saba kwa tuhuma za kukutwa wakijihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya aina ya Heroine mapema wiki.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Salum Hamduni amethibitisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao abapo amesema kuwa walikamatwa Agosti 12 mwaka huu saa 11.50 jioni wakijihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya.
Amesema jeshi la polisi limefanya msako wake na kuwakamata watuhumiwa hao wakiwa katika eneo ambalo linajihusisha na uuzaji wa dawa hizo.
“Chid Benz na wenzake wapo kituo cha Polisi cha Msimbazi ambapo tunaendelea na upelelezi na pindi utakapokamilika tutawafikisha Mahakamani na kiasi cha dawa zilizokamatwa zimepelekwa kwa Mkemia mkuu na itajulikana ni kiasi gani za dawa za kulevya zilizokamatwa” , alisema Hamduni.
Hamduni amesema jeshi hilo linafanya msako liweze kubaini mtandao mzima unaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya na watumiaji ili kuhakikisha wote wanachukuliwa hatua na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
Pamoja na hayo tukio hilo la kukamatwa kwa Chid Benz limetokea ikiwa ni muda mfupi tangu arudi kwenye muziki na kukuri kuachana na matumizi ya dawa za kulevya ambazo zilimfanya akapotea kwenye 'game'.
Hata hivyo kumbukumbu zinaonyesha kuwa hii siyo mara ya kwanza kwa msanii huyo kukamatwa akijihusisha na dawa za kulevya, itakumbukwa Oktoba 2014, Rapa huyo alikamatwa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) jiji la Dar es Salaam akiwa na dawa za kulevya, akijaribu kuvuka nazo kwenda mkoani Mbeya kushiriki tamasha la 'Instagram Party' akiwa na msanii Shetta.
Kwa sasa Chid ana wimbo mmoja mpya ' Muda' unaofanya vizuri aliyoshirikiana na mkongwe Q Chief.

Maoni