Ndani ya masaa 24 yajayo usajili wa wachezaji hawa unaweza kuitikisa dunia

Alhamisi usiku ndio dirisha la usajili barani Ulaya linafungwa na timu zote kwa sasa zinapigana vikumbo vya dakika za mwisho mwisho kununua wachezaji wapya kabla ya usiku huo wa Alhamisi, lakini hawa wafuatao usajiili wao unaweza kuitikisa dunia.

Phellipe Coutinho. Huu ndio usajili ambao unapewa nafasi kubwa sana kutokea, Coutinho hakuwa mazoezini na Liverpool wala kucheza mchezo wowote katika ligi kuu nchini Uingereza lakini ameonekana akipasha na timu yake ya taifa huku tetesi za uhamisho wake kwenda Barcelona zimezidi kushika kasi na inaonekana hilo linaweza tokea huku Barca wakiweka mzigo wa £125m.

Diego Costa. Alipewa nafasi ya kutafuta timu mpya baada ya maisha ndani ya klabu ya Chelsea kuonekana kumuendea mlama, Costa hadi sasa hajapata timu lakini ameweka wazi kwamba mapenzi yake yapo Athletico Madrid na huko ndiko anakotamani kwenda kabla ya siku ya Alhamisi na taarifa zaidi zinadai Chelsea na Athletico wanakaribia kukamilisha dili hilo

Kylian Mbappe. Jezi yake ameshakabidhiwa Jovetic huku inasemekana ameshawaambia rafiki zake katika kambi ya timu ya taifa ya Ufaransa kwamba anakwenda PSG huku akiwahakikishia kwamba usajili wake utafanyika kabla ya usiku wa Jumatano, Psg wanamchukua Mbappe kwa mkopo lakini wana makubaliano ya kumnunua hapo baadae.

Alexis Sanchez. Taarifa mpya zilizotoka hii leo zinadai kwamba klabu ya Manchester City imerudi tena kwa Sanchez na sasa wanataka kutoa pesa pamoja na Raheem Sterling ili kumnasa Sanchez, kipigo cha bao 4 toka kwa Liverpool kilionesha kumsononesha sana Sanchez  na anaweza kuondoka.

Thomas Lemar. Monaco wamesisitiza bila £60m Lemar hauzwi, mzee Wenger anamuhitaji Lemar lakini Liverpool wanatajwa kukaribia kukamilisha usajili huu, Monaco inasemekana wameanza kutafuta mbadala wa Lemar kwani tayari wameonekana kukubali wanamkosa Lemar.

Virgil Van Djik. Kama kuna mlinzi aliyetajwa sana katika kipindi hiki cha usajili baasi ni mlinzi huyu wa Southampton, walianza Chelsea baadae tetesi zikazimwa, wakaja Arsenal na sasa wamekuja Liverpool, anatajwa kuwa na thamani ya £70m na Liverpool wanaonekana wako tayari kutoa kiasi hicho pesa.

Maoni