Taarifa ya Msuva na Farid kutoonekana Stars hadi sasa

Inawezekana watu wengi wanajiuliza mbona Farid Musa anaecheza Tenerife, Hispania na Simon Msuva wa Difaa El Jadid ya Morocco hawaonekani kwenye mazoezi ya timu ya taifa ‘Taifa Stars’? Wakati tayari wachezaji wengine wapo kambini wakiendelea na mazoezi kuelekea mchezo wa kirafiki wa kalenda ya FIFA dhidi ya Botswana siku ya Jumamosi September 2, 2017.

Kocha mkuu wa Stars Salum Mayanga amefaganua ni kwa nini hadi sasa Msuva na Farid bado hawajaonekana kwenye mazoezi ya timu ya taifa licha ya kuwaita kwenye kikosi chake.

“Mpaka wakati huu tumebakiza wachezaji wawili ambao bado hawajafika lakini Simon tunakamilisha ujio wake kwa sababu alipata tatizo kwenye visa yake ambayo ilikwisha kule kwa hiyo leo tulikuwa tulibadilisha tiketi yake kwa mara ya tatu lakini mpaka saa 5 ahubuhi kulikuwa na uhakika wa kuanza safari yake leo”-Mayanga.

“Simon alikuwa na matatizo ya visa iliharibika kwa hiyo tulikata tiketi ya kwanza ikasumbua, tukakata ya pili, lakini leo mida ya saa 4 alishapata visa yake na tulituma tiketi ya kuanza safari mchana wa leo kuja huku kwa hiyo tunategemea kesho atawasili wakati wowote.”

“Farid amefika jioni hii na tayari yupo kambini, lakini Moreal ndiyo mtu pekee ambae tunadhani hato hudhuria kwenye mechi inayokuja lakini kwa asilimia 90 wachezaji wote wapo na tunaendelea vizuri na mazoezi na maandalizi yetu.”

“Ni matumaini yangu kesho mchana tutaendelea na mazoezi katika hali nzuri na keshokutwa asubuhi tutamalizia ili kusubiri mechi yetu dhidi ya Botswana.”

Maoni