VIKOSI VYA AU VYAISHIKILIA BARIIRE.

Vikosi vya Umoja wa Afrika (AU) na serikali ya Somalia vimeuteka mji wa Bariire, wenye kituo cha mkakati cha wapiganaji wa al-Shabab kusini mwa nchi hiyo, maafisa wa serikali na mashuhuda wa tukio hilo wamesema Jumamosi.
Makamanda wa vikosi hivyo wamesema kuwa kikundi cha al-Shabab kiliukimbia mji huo kufuatia mapigano makali nje ya eneo la mjini ambapo vikosi vya pamoja viliushambulia kutoka pande tatu.
Bariire ni moja ya mji mkubwa unaokaliwa na al-Shabab upande wa kusini na uko kilometa 45 (maili 27) kutoka Mogadishu, makao makuu ya Somalia.
Raia saba waliuawa na wengine wanne kujeruhiwa wakati gari ndogo iliyokuwa imewabeba raia hao kukanyanga bomu wakati wakikimbia kutoka mji huo, Abdinasir Alim Ibrahim aliiambia VOA. Lakini Ibrahim aliweza kuthibitisha vifo vya raia wanne na watu watatu kujeruhiwa.
Walioshuhudia tukio hilo wameiambia VOA kwa sharti la kutotajwa majina yao kuwa waliona kiasi cha dazeni moja ya maafisa wa kijeshi weupe wanaovisaidia vikosi vya Somalia na AU walipokuwa wanaingia katika mji huo.
Maafisa wa serikali ya Somalia wamethibitisha kuhusika kwa wanajeshi wa kigeni katika shambulizi hilo lakini walikataa kusema chochote kuhusu mataifa yao.

Maoni