Wanawake washinda nyadhfa za Ugavana Kenya

Aliyekuwa waziri wa ardhi nchini Kenya Charity Ngilu ni miongoni mwa wanawake watatu nchini Kenya wanaotarajiwa kuwa magavana wapya wa kaunti zao.
Ngilu ambaye aliwania wadhfa huo katika kaunti ya Kitui nchini Kenya kupitia chama Nark alimshinda Gavana Julius Malombe kwa wingi wa kura.
Mgombea mwengine mwanamke ambaye ameshinda wadhfa wa Ugavana ni aliyekuwa naibu wa spika bungeni Dkt Joyce Laboso .
Laboso amemshinda gavana Isaac Rutto ambaye hivi majuzi alikuwa miongoni mwa viongozi wakuu wa muungano wa upinzani Nasa.
Mwanamke huyo ambaye alikuwa akigombea wadhfa huo kupitia chama tawala cha Jubilee alikuwa ameshutumiwa na mpinzani wake aliyemtaka kuwania ubunge katika eneo la Nyanza alikoolewa.
Mgombea mwengine ni Anne Waiguru ambaye wakati mmoja alihudumu kama waziri wa maswala ya ugatuzi .
Waiguru ambaye alilazimika kujiuzulu katika wadhfa huo kutokana na madai ya ufisadi yaliomkabili anaendelea kupata ushindi dhidi ya Martha Karua aliyewahi wakati mmoja kugombea urais mbali na kuwa waziri..

Maoni