Chadema Wamjia Juu IGP Sirro Kutekeleza Majukumu Yake Ikiwemo Upelelezi na Kuacha Kukataza Kujadili Suala la Lissu


CHAMA cha Demokrasia na Maendelo (Chadema) kimemtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Nyakoro Sirro kutekeleza majukumu yake ikiwemo kufanya upelelezi na kuhakikisha wanawatia nguvuni walioshiriki katika tukio la kumshambulia Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu ambaye amelazwa jijini Nairobi akitibiwa.
Akizungumza na wanahabari leo katika ofisi za Makao Makuu ya CHADEMA Kinondoni Dar es Salaam leo, (Jumatano), Oktoba 11, 2017, Mwanasheria wa chama hicho, John Mallya amesema:
“Wakati wanasiasa, wanasheria na wananchi wa Jimbo ambalo Tundu Lissu anatoka, wakijadili kuhusu mustakabali wa kiongozi wao aliyejeruhiwa, Sirro anapaswa kunyamaza na kufanya kazi ya upelelezi. Kitu tunachotaka kusikia kutoka kwake apeleke watu mahakamani, na si kuwaambia wananchi mitandaoni wanyamaze, kufanya hivyo anakiuka masharti ya ibara ya 18 ya katiba ya nchi,” alisema Mallya.
“Aliyepigwa risasi zaidi ya 30 pale Dodoma si mbuzi, ni binadamu, kwa nini tusimjadili?” alihoji Mallya na kuongeza, Sirro alipaswa achukue advantage (fursa) ya mijadala hiyo ya wanasheria kuifanyia upelelezi.
Aidha Mallya amewataka wananchi, wanansheria na wanasiasa kuendelea kujadili suala la Lissu huku akidai kuwa, kwa kufanya hivyo hawavunji sheria yoyote ya nchi na badala yake inaweza ikawa chanzo kizuri cha kuwapata watuhumiwa wa tukio hilo.
Kuhusu hali ya afya ya Lissu, Katibu Mkuu wa Chadema-Zanzibar, Salum Mwalimu, amesema hivi karibuni watatoa taarifa rasmi ya maendeleo ya mbunge huyo.

Maoni