Mwanafunzi Aliyekutwa na Bomu, Wenzie Wamefikishwa Mahakamani


Watu watatu akiwemo mchimba makaburi, Mohammed Maganga mwenye umri wa miaka 61, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi wa kukutwa na Bomu la kurusha kwa mkono.

Mbali ya mchimba makaburi, Maganga wengine ni mfanyabiashara Rahma Mwinyi mwenye miaka 37 na mwanafunzi Almas Sued.

Washtakiwa hao walisomewa makosa yao na Wakili wa Serikali, Adolf Mkini mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri ambapo wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi.

Inadaiwa September 16, 2017 wakiwa maeneo ya Upanga DSM washtakiwa walikutwa na silaha moja aina ya Uzigun bila kibali.

Pia inadaiwa kati ya September 16, 2017 pia walikutwa na risasi 167 bila kibali huku wakidaiwa katika tarehe hiyo walikutwa na Bomu la kurusha kwa mkono (Hand grenade) bila kibali.

Baada ya kusomewa makosa hayo, washtakiwa walikana makosa na Wakili Mkini alidai upelelezi wa kesi hiyo unaendelea ambapo Wakili wa utetezi Mluge Karoli alidai kuwa kesi hiyo inadhaminika, hivyo washtakiwa wadhaminiwe.

Hata hivyo, Wakili Mkini alidai watuhumiwa wanashtakiwa kwa kosa la uhujumu hivyo hawapaswi kupewa dhamana.

Kutokana na hatua hiyo, Hakimu Mashauri alitoa uamuzi ambapo alisema kesi hiyo inadhaminika na washtakiwa wanapewa masharti ya kuwa na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya Tsh Milioni 20 kila mmoja lakini washtakiwa hao hawakutimiza masharti, isipokuwa Swedi ambapo kesi imeahirishwa hadi October 23, 2017.

Maoni