Refa wa kike akifanya yake.
WIKIENDI hii Ligi Kuu Bara inaingia raundi ya sita na timu zote zinazoshiriki ligi hiyo kupambana kwa nguvu kuhakikisha zinapata matokeo mazuri ili ziweze kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kutwaa ubingwa wa ligi hiyo msimu huu.
Mpaka kufikia raundi ya tano, zipo timu zilizofanya vizuri na nyingine vibaya, lakini hivyo ndivyo mchezo wa soka ulivyo kwani una matokeo ya aina tatu, kushinda, sare na kufungwa.
Timu ya Simba ndiyo inayoongoza msimamo wa ligi ikiwa na pointi 11 sawa na Mtibwa Sugar na Azam lakini zote zinatofautiana kwa idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa yaani GD. Simba imefunga mabao 14, Mtibwa (5) na Azam manne.
Hata hivyo, ili kuifanya ligi yetu iweze kukua ni lazima Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ambalo ndilo baba wa soka hapa nchini lisimamie mambo ya msingi zaidi kuhakikisha kila kitu kinachoihusu ligi hiyo kinafanyiwa kazi haraka sana.
Katika misimu iliyopita yamekuwa yakisemwa mengi kuhusiana na waamuzi kuwa ndiyo adui namba moja wa maendeleo ya soka hapa nchini.
Hali imesababisha baadhi yao kutazamwa tofauti na jamii inayowazunguka kwa sababu tu ya tuhuma hizo ambazo wamekuwa wakitumiwa mara kwa mara.
Wengi wao walituhumiwa kwa kujihusisha na vitendo vya rushwa ili waweze kuzisaidia baadhi ya timu kupata matokeo mazuri na kuzikandamiza nyingine ambazo hazikuwa na uwezo wa kuwahonga.
Ukiachana na vitendo hivyo pia kuna jambo moja ambalo mara nyingi limekuwa likipigwa kelele na mara kwa na waamuzi wa kike kuhusiana na changamoto mbalimbali ambazo wamekuwa wakikumbana nazo uwanjani lakini pia nje ya uwanja.
Siku moja nikiwa katika harakati zangu za kazi, nilikutana na mwamuzi mmoja wa ligi kuu wa kike na katika mazungumzo naye aliniamba kuwa anatamani kuachana na soka kutokana na changamoto nyingi anazokumbana nazo kutoka kwa wachezaji lakini zaidi ni kwa viongozi.
Alidai kuwa waamuzi wengi wa kike utu wao unadhalilishwa sana na zaidi wanaoongoza kufanya hivyo ni viongozi wao ambao ni wanaume.
Ili mwamuzi wa kike aweze kupanda daraja atakumbana na visa vingi sana na kama atakuwa mwepesi kukata tamaa basi anaweza kuishia njiani.
Lakini pia kunadaiwa kuwa kuna viashiria vya rushwa ambavyo TFF na bodi ya ligi wanatakiwa kuhakikisha kuwa wanazuia mianya hiyo.
Kutokana na hali hiyo ndiyo maana mpaka sasa katika waamuzi wengi kike waliyokuwa mahiri enzi hizo kwa kuchezesha soka na ambao waliaminika kuwa watafika mbali hawapo tena.
TFF inatakiwa kuliangalia suala hilo kwa kina kwani siyo zuri na linachafua taswira nzima na mchezo wa soka hapa nchini.
Kwa muda mrefu sana Tanzania haikuwahi kutoa mwamuzi katika fainali za mataifa ya Afrika na Kombe la Dunia. Ni hivi karibuni tu mwamuzi wa kike Jonesia Lukyaa aliweze kuitoa kimasomaso baada ya kuteuliwa kuchezesha Fainali za Mataifa ya Afrika kwa wanawake zilizofanyika mwaka jana huko nchini Cameroon tunafikiri ni jambo jema, hivyo ni kazi ya TFF kuhakikisha wanapatikana wengi zaidi wa kwenda huko.
Lakini pia hivi karibuni amechaguliwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) kwenda kuchezesha Fainali za Kombe la Dunia kwa Wanaweka chini ya miaka 20 zitakazofanyika nchini Ufaransa.
Ninaimani kubwa na TFF chini ya Rais Wallace Karia kuwa itasaidia kukuza kiwango cha waamuzi wanawake wengi zaidi ambao ndiyo watakaokwenda kuchezesha soka huko majuu na kuitangaza nchi yetu kimataifa zaidi.
Maoni
Chapisha Maoni