Walionusurika wa Ajali ya Daladala Iliyotumbukia Ziwa Victoria Wasimulia na Kumtupia Lawama Dereva

Walionusurika ajali ya daladala iliyotumbukia Ziwa Victoria, wamesema iwapo dereva angesikiliza ushauri madhara yasingekuwa makubwa.

Akizungumza katika Hospitali ya Bukumbi Mission wilayani Misungwi alikolazwa, Yohana Ngabula (28) mkazi wa Kijiji cha Buyagu wilayani Sengerema amesema amepoteza mama na dada katika ajali hiyo.

Ngabula amesema walikuwa wakitoka jijini Mwanza kufuatilia mafao ya baba yao katika ofisi za Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF).

“Nilimshauri dereva agonge hata gari lililokuwa mbele yake badala ya kulielekeza ziwani lakini hakusikia mwisho wake ndiyo hayo yaliyotokea,” amesema.

Amesema baada ya gari kutumbukia ziwani alipasua kioo na kutoka ndipo walipofika vijana wakamuokoa.

Majeruhi mwingine mkazi wa Ibisabageni, Paulo Lazaro ambaye ni mwalimu wilayani Sengerema amesema, “Tulimshauri dereva agonge vitu nchi kavu kuliko kuipeleka gari majini lakini hakusikiliza ushauri wetu, pengine tungepona wengi zaidi.”

Maoni