‘Azam FC itaibuka na ushindi v Singida Utd’

NAHODHA wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati Azam FC, Himid Mao ‘Ninja’, anaamini ya kuwa kikosi hicho kitatinga tena fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi kwa kuichapa Singida kesho Jumatano.

Mabingwa hao watetezi wa michuano hiyo wanacheza na Singida United katika mchezo wa nusu fainali ya michuano hiyo, unaotarajia kufanyika Uwanja wa Amaan, Zanzibar kuanzia saa 2.15 usiku.

Mao aliuambia mtandao rasmi wa klabuwww.azamfc.co.tz kuwa anakiamini kikosi hicho pamoja na wachezaji wenzake huku akidai wanajua namna ya kupambana na kupata matokeo katika mechi ya aina hiyo.

“Tunamshukuru Mwenyezi Mungu tumemaliza mazoezi yetu salama, mazoezi leo yalikuwa mazuri sana hata wachezaji wameonyesha morali kubwa, ni kitu kizuri kuelekea katika mchezo wetu wa kesho kwa hiyo naamini kesho tutaweza kupata matokeo mazuri na pia tutaweza kucheza mpira mzuri zaidi.

“Mechi itakuwa ya ushindani sana hatujacheza na Singida sana tangu imepanda daraja tumecheza nayo mara moja tu katika mchezo wa ligi ambao ulikuwa sare (1-1) kule kwao, lakini hali ya uwanja haikuwa nzuri sana mchezo haukuwa wa kuvutia sana, lakini kesho naamini uwanja mzuri, timu zote zinawachezaji wazuri timu itakayokuwa na uwezo zaidi itaweza kuibuka na ushindi, naimani Azam FC itaweza kufanya hivyo,” alisema.

Nyota huyo ambaye pia ni Nahodha Msaidizi wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, alisema kuwa mechi hiyo ni njia ya kwenda kwenye fainali na kudai ni mechi muhimu kwao kushinda zaidi ya fainali kwa kuwa ili uweze kuingia fainali lazima ushinde mtanange huo.

“Mashabiki wasapoti, ambao wako Dar es Salaam kama wanaweza kuja kuangalia mpira waje na waliokuwa hapa Zanzibar waje kuangalia mpira na hata ambao sio mashabiki wa Azam na hata ambao sio wa Singida pia, nafikiri mashabiki wote wa mpira, mpira wa kesho ni mzuri kila mtu anastahili kuja kuuona na kusapoti,” alisema.

Kocha naye anena

Akizungumzia kiufundi Kocha Msaidizi wa Azam FC, Idd Nossor Cheche, amesema kuwa wachezaji wote wapo kwenye hali nzuri kuelekea mtanange huo huku akiwaambia mashabiki wajiandae kufurahi kwa ushindi watakaupata.

“Wachezaji wako vizuri, wako na furaha, wako vizuri kiakili, kimwili na wako tayari kupambana, tunawaambia mashabiki wetu waje kutusapoti sisi tuko kwa ajili yao kuhakikisha wakija uwanjani waondoke na furaha kama walivyotarajia,” alisema.

Mwaka jana wakati Azam FC ikitwaa ubingwa, Azam FC iliichapa Taifa ya Jang’ombe bao 1-0 kwenye nusu fainali kabla ya kupata ushindi kama huo katika fainali kwa kuifunga Simba.

Nusu fainali ya kwanza itayoanza saa 10.30 jioni itawahusisha URA ya Uganda itakayokipiga na Yanga.

Maoni