AJIB,NGOMA NA KAMUSOKO KUIKOSA LIPULI.

Mkuu wa kitengo cha habari na mawasiliano wa klabu ya Dar Young Africans Disma Ten, ameweka wazi kuwa Ibrahim Ajib na Haji Mwinyi wataukosa mchezo wa ligi kuu soka Tanzania Bara dhidi ya Lipuli

Ten amesema wachezaji hao bado wanamajeraha na hivyo hawatakuwa sehemu ya mchezo huo ambao utafanyika katika uwanja wa Samora mjini Iringa siku ya Jumamosi ya Januari 3.

“Mbali na Ajib na Mwinyi pia tutaendelea kuwakosa wachezaji ambao wana majeraha muda mrefu sasa akiwemo Thaban Kamusoko na Donald Ngoma, lakini matayarisho kwa upande wetu tayari matayarisho yamekamilika,” amesema.

Lipuli nao wamejiandaa

Amesema hawataidharau Lipuli kwa namna yoyote ile kwani ni timu ambayo nayo imejiandaa na inataka ushindi tena ikiwa katika ardhi ya nyumbani kwao, na amewaomba mashabiki wa Yanga waliokaribu na Iringa kujitokeza kwa wingi kuishangalia timu yao.

“Mwalimu (George Lwandamina) amenihakikishia kwamba timu itacheza mchezo mzuri na matokeo ndani ya uwanja ni lazima yaheshimiwe tunaweza kuiandaa timu kwa ajili ya kupata matokeo, sisi tupo imara ila naamini mchezo utakuwa mzuri kwani kila timu ina kiu ya kupata matokeo mazuri,” Ten amesema.

Katika mchezo wa duru ya kwanza uliopigwa katika uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam timu hizo zilitoka sare ya bao 1-1 ambapo bao la Lipuli lilifungwa na Seif Abdlah Karihe huku la Yanga likifungwa na Donald Ngoma.

Maoni