KLABU YA YANGA SC LEO INATIMIZA MIAKA 83 NA HII NDO HISTORIA YAKE

Yanga leo inasherehekea miaka ya 83 ya kuzaliwa kwake.
Kwa ufupi kabisa tujikumbushe Historia ya kuundwa kwa klabu hii kongwe na Baba wa soka Tanzania Bara.
Ingawa historia inasema Yanga ilianzishwa mwaka 1935 na Simba mwaka 1936, lakini ukizama ndani utagundua kwamba, huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa utani na upinzani wa jadi baina ya miamba hiyo ya soka nchini.
Kulikuwa kuna timu inaitwa New Youngs ambayo mwaka 1935 ilisambaratika na baadhi ya wachezaji wake wakaenda kuunda timu iliyokuwa Sunderland, ambayo hivi sasa inajulikana kama Simba.
Kabla ya kutokea vurugu zilizoisambaratisha New Youngs vijana wa Dar es Salaam walikuwa na desturi ya kukutana viwanja vya jangwani kufanya mazoezi na baada ya muda wakaamua kuunda timu yao, waliyoipachika jina Jangwani Boys.
Ndani ya kipindi kifupi timu hiyo iliteka hisia za wengi, waliojitokeza kujiandikisha uanachama wa klabu hiyo, miongoni mwao waliovutiwa na uanachama wa klabu hiyo ni Tabu Mangala (Sasa marehemu) na ilipofika mwaka 1926 walifanya mkutano wa kwanza katika eneo ambalo hivi sasa kuna shule ya sekondari ya Tambaza.
Miongoni mwa yaliyojadiliwa kwenye mkutano huo ni kuiboresha timu hiyo ambayo wachezaji wake wengi walikuwa wafanyakazi wa bandarini na mashabiki wake wengi walikuwa wabeba mizigo bandarini.
Baada ya mkutano huo, timu ilibadilishwa jina na kuwa Navigation, iliyotokea kuwa moto wa kuotea mbali katika timu za waafrika enzi hizo, kabla ya uhuru wa Tanganyika.
Timu kama Kisutu, Kitumbini, Gerezani na Mtendeni zilikuwa hazifui dafu kwa wana wa Jangwani hao.
Ikiwa inatamba kwa jina la Navigation, wanachama wa timu hiyo walikuwa wanatembea kifua mbele na kuwatambia wapinzani wao, kwamba katika kipindi hicho wao ndiyo zaidi, kwa sababu Italia ilikuwa inatamba kwenye ulimwengu wa soka, wanachama wa timu hiyo nao waliamua kuibadilisha jina timu yao na kuiita Italiana.
Italiana FC ilipata mafanikio ya haraka na haikushangaza ilipopanda ligi Daraja la pili kanda ya Dar es Salaam.
Mwanzoni mwa miaka ya 1930 Italiana waliamua kuachana nalo mapema kabla ya kuingia kwenye ligi hiyo, hivyo wakaanza kujiita New Youngs.
Kila ilipokuwa ikibadilisha jina, ilikuwa ikifanya vitu vipya pia, kwani wakiwa na jina la New Youngs waliweza kutwaa kombe la Kassum, lililoshirikisha timu mbalimbali za Dar es Salaam.
Hatimaye ukawadia mwaka mbaya kwa New Youngs 1935 wakati baadhi ya wachezaji walipojitoa na kwenda kuanzisha Sunderland mwaka 1936.
Kwa sababu hiyo, waliobaki wakaamua kubadili jina na kuwa Young Africans jina ambalo mashabiki wake wengi walishindwa kulitamka vizuri hivyo kujikuta wakisema Yanga.
Miaka ya 83 baadaye leo, ni timu ya kihistoria Tanzania ikiwa inaongoza kutwaa ubingwa wa ligi kuu Tanzania Bara kwa mara 27.
Pongezi nyingi ziwaendee wachezaji wote waliopata kuichezea timu hiyo kuanzia enzi za Jangwani Boys, Navigation, Italiana, New Youngs hadi leo hii ikijulikana kama Yanga ingawa katika cheti chake cha usajili inafahamika kama Dar Young Africans.
Mafanikio ya Yanga ndani ya miaka 83 hayakuja hivi hivi bila kuwapongeza viongozi ambao walihakikisha timu hiyo inasimama kidete.
Viongozi wa enzi hizo hadi leo hii wanastahili pongezi kwa kuiwezesha kutwaa mara nyingi ubingwa wa nchi.
Shukrani nyingine ziwaendee wanachama, wapenzi na mashabiki, bila kuwasahau waandishi wa habari, bila hamasa zao sidhani kama Yanga ingeweza kufika hapo ilipo
Yanga inajivunia kuwa Baba wa soka Tanzania Bara. Kama si Yanga kusingekuwa na Simba! Hii Simba imetoka kwenye ubavu wa Yanga!
Yanga inajuvunia kuwa na mashabiki wengi mmoja wapo ni aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania awamu ya nne Dk Jakaya Mrisho Kikwete ambaye mwaka 1976 alikuwa mwenyekiti wa kamati ya usajili wa klabu hiyo na kufanikisha usajili wa Shaaban Katwila.

Maoni