Leo Jumamosi 24 February 2018 Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Kusini Unguja Ndg. Latifa Juakali amekizindua rasmi kitabu cha HATUBEBI MABEGI kwa upande wa Tanzania visiwani.
Uzinduzi huo ulioenda sambamba na utoaji semina elekezi kwa wajumbe wa kamati za utekelezaji za jimbo, wilaya na Mkoa ulihusisha mada mbalimbali ikiwemo ya hatubebi mabegi iliyotolewa na Mwenyekiti wa UVCCM Kata ya Chamazi Ndg. Nasri Mkalipa ulifanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja.
Akizungumza wakati wa utoaji wa mada ya hatubebi mabegi Ndg. Mkalipa aliwataka vijana kuwa na msimamo, uthubutu, ubunifu na mshikamano ili kuweza kusonga mbele na hatimaye kuweza kuaminiwa na kupata nafasi za juu zaidi ya walizonazo.
"Neno hatubebi Mabegi linamtaka kijana kuthubutu, kuwa mkweli, mbunifu, kutokuwa muoga katika mambo yenye tija kwa CCM na Jumuiya yetu" alisema Mkalipa.
"Kwa hiyo kijana bila kujali nafasi uliyonayo thubutu kufanya mambo mazuri yatakayoacha alama na kukumbukwa vizazi na vizazi" alisema Mkalipa.
"Mwenyekiti wetu UVCCM Taifa Ndg. KHERI JAMES anapambana usiku na mchana kuhakikisha Jumuiya yetu inakuwa ni yenye tija nasisi hatuna budi kufanya kazi kwa bidii ili kuileta tija hiyo kwa wananchi" alisema Mkalipa.
Akizungumza wakati wa kuzindua kitabu hicho Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Kusini Unguja Ndg. Latifa Juakali aliwataka vijana wa Mkoa wa Kusini Unguja kuwa wathubutu, wabunifu, wasio na uoga pia kukisoma na kukielewa kitabu cha Hatubebi Mabegi kwani kitawasaidia kujua lipi baya lipi zuri.
Pia alimpongeza Ndg. Mkalipa kwa kuandika kitabu chenye kutia ujasiri, uthubutu na nguvu ya kufanya kazi kwa bidii na hatimaye kutekeleza ilani ya CCM.
Maoni
Chapisha Maoni