RC MAKONDA ATEMBELEA SHULE ZILIZOONGOZA KWA UANDIKISHAJI MKUBWA WA WANAFUNZI WA DARASA LA KWANZA TANZANIA NZIMA, AAGIZA UJENZI WA SHULE MPYA

Mkuu  wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda leo amefanya Ziara kwenye Shule ya Msingi Mbande na Maji Matitu zilizopo Manispaa ya Temeke ambazo zimeongoza kwa kuandikisha idadi kubwa ya Wanafunzi wa Darasa la Kwanza kuliko shule yoyote Tanzania na kusababisha mlundikano mkubwa wa Wanafunzi Darasani.

Kwa Shule ya Msingi Mbande imeandikisha zaidi ya Wanafunzi 1,130 na kusababisha upungufu wa Vyumba vya Madarasa 115 na Matundu ya Vyoo 270 na Madawati 308 huku shule ya Msingi Maji Matitu nayo ikiandikisha zaidi ya Wanafunzi 976 hali iliyosababisha baadhi ya Wanafunzi kukaa kwenye Sakafu, Chini ya miti na Msongamano mkubwa Madarasani.

Hali hiyo imemfanya 
RC Makonda kufika kwenye shule hizo ili kujua mpango wa Manispaa katika kutatua changamoto hiyo iliyosababishwa na nia njema ya wazazi kuitikia wito wa Serikali ya awamu ya Tano chini ya Rais Magufuli ya kutoa elimu Bure.

Kama ilivyo kawaida ya RC Makonda kutafuta majibu kwenye Changamoto amesema serikali inaanza Mara moja ujenzi wa shule tatu Mpya ambapo Shule mbili zitajengwa Maji Matitu na Moja Mbande.

Aidha RC Makonda amesema makadirio ya uandikishwaji wa wanafunzi wapya darasa la kwanza kwa Wilaya ya Temeke ilikuwa wanafunzi 7,800 lakini idadi imepanda hadi kufikia Wanafunzi 28,824 na idadi inazidi kuongezeka kila kukicha huku Mkoa ukiwa na malengo ya kuandikisha wanafunzi 78,000 lakini hadi sasa wamefanikiwa kuandikisha Wanafunzi 86,000.

RC Makonda amesema mwitikio huo wa wananchi kwenye elimu ni faida kubwa kwakuwa ndio ukombozi wa familia maskini hivyo amewasihi wananchi kuchangamkia fursa ya iliyotolewa na Rais Magufuli ya Elimu Bure.

Hata hivyo RC Makonda amewahimiza 
Wananchi kuunga mkono ujenzi wa shule hizo tatu mpya kwa kujitolea vifaa mbalimbali kama Saruji, Mchanga,  Nondo, Kokoto, Mabati, Rangi, Mbao na nguvu kazi ya Watu ili wanafunzi wasome katika mazingira bora. 

Kwa upande wake kaimu afisa elimu ya msingi manispaa ya Temeke Bi. Sylvia Mtasingwa amesema licha ya shule ya Mbande kuwa na idadi kubwa ya Wanafunzi imeendelea kufanya vizuri kwenye matokeo ya mitihani.


UKITAKA KUMKOMBOA MTOTO WA FAMILIA MASKINI MPATIE ELIMU, KWA PAMOJA TUSHIRIKIANE KUBORESHA MAZINGIRA YA ELIMU DAR ES SALAAM. 

Maoni