DKT.MWIGULU AAGIZA WANAOPANGA MIPANGO YA MAANDAMANO WAKAMATWE


Na Globu ya Jamii

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dk.Mwigulu Nchemba amesema amemuagiza na kumuelekeza Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Simon Sirro kuwakamata watu wote ambao wamepanga njama za kutaka kuwauwa watanzania katika maandamano ambayo wameyapanga kuyafanya Aprili 26 mwaka huu.

Dk.Mwigulu ametoa maelekezo hayo wakati alipokuwa akitoa salamu zake kwa Rais Dk.John Magufuli aliyopo mkoani Singida katika ziara yake ya kikazi ambapo jana amezindua kiwanda cha Alizeti mkoani humo.Amesema lengo la maandamano hayo ni kutaka kuchafua taaswira ya nchi na tayari ameshatoa maelekezo kwa IGP Sirro.

"Njama hiyo tumeiona na mimi nimemuelekeza IGP Sirro kwamba hata kupanga njama ya kuua ni kosa, wachukue hatua kwa wale watu wanaopanga mipango ya aina hiyo na kuchafua taswira ya nchi yetu ama kwa mipango yao au ya wale wanaowatuma." Watu wanataka mikusanyiko ili wafyatue na kuuwa watu  ili kuchafua taswira ya nchi yetu na tunayo mifano wa maeneo waliwahi kufanya jambo la aina hiyo na hatua zitachukuliwa", amesema Dk.Mwigulu.

Pamoja na hayo, Dk.Mwigulu ameendelea kwa kusema "Mhe. Rais ndio maana unaona vinyago vinyago vingi hivi kama hivi juzi alitokea kijana mdogo amesema ametekwa, eti ametekwa na akapata muda wa kutafuta pafyumu na nguo za kubadilishia kule atakapokuwa ametekwa. Unatowa wapi muda wa kujiandaa ?

"Watu wanatafuta njia za kuchafua taswira ya nchi yetu, na jambo hili Mhe. Rais kama ambavyo ulishatoa maelekezo, si jambo ambalo tutacheza nalo wala mjadala, hakuna sababu ya maandamano wala hakuna sehemu ya kuandamania na hakuna ruhusa ya kuandamana,"amesisitiza.Pia Dk.Mwigulu amesema endapo ikatokea hata watu wakaandamana ndani ya nyumba zao bado sheria itachukua mkondo wake dhidi ya watu hao.

"Ikitokea hata watu wakaandamana ndani ya nyumba wakazunguka kitanda na akatokea mtu akaumia, yule aliyeitisha waandamane pale atakuwa nala kuajibika kwasababu watu wanafanya mzaha na maisha na dira ya nchi yetu ambapo Rais umejitoa muhanga kwa ajili ya kutengeneza urithi wa watoto wa Tanzania",amesisitiza Dk. Mwigulu.

Kwa upande mwingine, amesema yeyote atakayethubutu kutaka kuharibu Taifa la Tanzania kwa kufanya vitendo vya uovu hawatoweza kumuacha salama.

Maoni