KESSY: NAJIANDAA KUSHANGILIA UBINGWA BARA

BEKI wa pembeni wa Yanga, Hassan Kessy, amesema kuwa hajutii kutua kuichezea timu hiyo, huku akitamba kuwa, anajiandaa kubeba ubingwa wa Ligi Kuu Bara kwa mara ya pili mfululizo.

Kessy alitoa kauli hiyo baada ya timu yake hiyo kuifikia Simba kwa idadi ya pointi 46, baada ya awali kuachwa kwa pointi saba.
Beki huyo, tayari amebeba taji hilo la ubingwa mara moja tangu ajiunge nayo msimu uliopita akitokea Simba baada ya mkataba wake kumalizika.

Akizungumza na Championi Jumatatu, Kessy alisema amebeba ubingwa huo wa ligi kwa mara ya kwanza akiwa na Yanga huku akiamini kubeba kwa mara ya pili msimu huu, inawezekana.

“Simba watajutia sisi kuwafikia kwa pointi 46 walizokuwa wanaongoza katika msimamo wa ligi na malengo yetu ni kuutetea ubingwa huo tunaoushikilia katika msimamo.

“Kama tumeweza kuzifikia pointi zao, tutashindwaje kuwapita na kukaa kileleni na mwisho wa ligi tunatangazwa kuwa ni mabingwa kwa mara ya nne mfululizo?
“Na hilo linawezekana kwetu kwani tayari wachezaji wetu muhimu waliokuwa kwenye majeraha wameanza kupona na kurejea uwanjani kama Kamusoko (Thabani), Dante (Andrew Vincent), Ngoma (Donald) na Tambwe (Amissi),” alisema Kessy.

Maoni