NIDA KUZINDUA USAJILI WA VITAMBULISHO VYA TAIFA KIGOMA, RUKWA NA KATAVI

MAMLAKA ya Vitambulisho vya Taifa(NIDA)  inatarajia kuzindua usajili na utoaji wa  vitambulisho hivyo katika mikoa mitatu ya Katavi, Kigoma na Rukwa.

Pia  NIDA  kwa kushirikiana na  Wizara ya Madini , imeanza  kuwasajili watu wote watakaoishi, kufanya kazi au biashara ndani ya eneo lililozungushiwa ukuta lenye madini ya TANZANITE huko Mererani mkoani Arusha.

Akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam, leo, Kaimu Ofisa Uhusiano  wa NIDA,  Rose Joseph, alisema   mpaka sasa mamlaka hiyo imaendelea  na  usajili na utoaji vitambulisho vya  uraia  katika mikoa 20.

“Hivi karibuni tutafanya uzinduzi katika mikoa mitatu iliyobaki ambayo ni Kigoma,  Rukwa na Katavi . Wananchi katika mikoa hii watakuwa na muda wa miezi mitatu wa kujisajili,  na hivyo  tutakuwa  tumeifikia nchi nzima,”alisema Rose.Ofisa huyo alisema  pia NIDA taangu Novemba   mwaka uliopita  ilianza  usajili wa mkupuo katika mikoa mbalimbali   na muda ulikuwa ukiongezwa  kadri ilivyokuwa uinaruhusu.

“Tayari baadhi ya mikoa imemaliza kazi ya kusajili  kwa mkupuo ikiwemo mikoa ya Mara na Iringa,”.alieleza  Rose.Alisema  katika kazi hiyo ya usajili NIDA kwa kushirikiana na Idara ya Uhamiaji  wanapeleka  maofisa hadi  ngazi ya kata na vijiji,  ili  kuhakikisha  kazi hiyo inakwenda kwa mchujo sahihi na wale wote wanaosajiliwa wawe na sifa  na vigezo kuwa raia  wa Tanzania. “Tunasajili  vitambulisho vya aina tatu ambavyo ni vya uraia, mkimbizi na mgeni na kumekuwa na ufanisi mkubwa,”alifafanua ofisa  uhusiano huyo.


Kaimu Ofisa Uhusiano Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) Rose Joseph akielezea mikakati ya kuzindua usajili wa vitambulisho Kigoma, Rukwa na Katavi sambamba na ndani ya mgodi wa Tanzanite.

Maoni