TELEVISHENI MWISHO SAA TATU USIKU -MKUU WA MKOA KUSINI PEMBA

Serikali ya mkoa wa kusini Pemba imewapiga marufuku wafanyabiashara na wamiliki wa mabanda ya video kutoonyesha tv zao kuanzia saa tatu za usiku ili kutoa nafasi kwa wanafunzi kujisomea na kujiepusha na matendo ya udhalilishaji yanayoweza kuepukika.

Akizungumza na walimu,wanafunzi na wazazi wa skuli ya Mtambile katika harambee ya uzinduzi wa mfuko wa uchangiaji wa ujenzi wa skuli hiyo Mkuu wa mkoa wa Kusini Pemba Mh Hemed Suleiman Abdalla amesema ni marufuku kwa mfanya biashara yeyote kuonyesha tv nje kuanzia saa tatu usiku na atakae kaidi agizo hilo atafutiwa leseni yake ya biashara.

'' Wazee munawachia hawa watoto wa kike saa tatu usiku wapo nje kwa
kisa nyumbani hakuna tv, kesho yake tunasikia mtoto amebakwa, nasema
kuanzia sasa wafanya biashara haturuhusu kuonyesha tv nje muda mkubwa kuanzia saa tatu usiku na atakae kaidi hili tutamshughulikia ipasavyo bora kinga kuliko tiba'' alisema mkuu wa mkoa huyo.

Akizungumzia juu ya suala la kushuka kwa ufaulu wa wanafunzi katika
skuli hiyo RC Hemed amesema kumechangiwa na utoro wa wanafunzi ulio
kithiri huku wazazi wakilikalia kimya suala hilo jambo ambalo linarejesha nyuma maendeleo ya skuli na Taifa kwa ujumla.

''Wazazi tulikuwa tunalalamika sana watoto wetu hawapasi , watoto
watoro na wazee tunanyamaza kimya nakuombeni sana wazee tubadilike
kwani mtoto bila elimu hakuna maendeleo''alisema RC Hemed.
Aidha amewataka wanafunzi wa kike kusoma kwa bidii kwani nafasi za
ajira zipo nyingi na kuwataka kuachana na kutamani ndoa za mapema.

Kwa upande wake Mwalimu Salum Yussuf Ali amesema suala la uoneshwaji wa tv za usiku limekuwa likirudisha nyuma sana maendeleo ya wanafunzi na kusema kuwa wanafunzi wanashindwa kufanya vizuri katika masomo yao na kujiingiza katika masuala ya starehe na anasa mambo ambayo ni adui kwa elimu .
''Sula ambalo mkuu wa mkoa kalizungumza linapaswa kupewa kipao mbele
na kila mtu na kufatiliwa kwa kina katika utekelezaji wake kwa
mafanikio yetu na watoto wetu''alisema mwalimu Yussuf.

Amesema iwapo suala la uoneshwaji wa tv za usiku na utoro kwa
wanafunzi yataondoshwa kutawafanya wanafunzi kujitambua na kufanya
vizuri katika mitihani yao ya Taifa.

Sambamba na hayo ametoa wito kwa wazazi na walezi kushirikiana na
walimu kikamilifu ili kuhakikisha watoto wanasoma vizuri na kuachana
na mambo yote yasiyo na maana kwao.

Maoni