CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) CHAELEKEZA KUTOLEWA KWA SHILINGI MILIONI 900 KWA AJILI YA MIKOPO KWA WANAWAKE WILAYA YA KINONDONI

 Tarehe 19 Mei 2018 Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia kwa Ndg. Humphrey Polepole, Katibu wa Itikadi na Uenezi kimeielekeza Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kutoa milioni 300 na kuagiza Mfuko wa Kujitegea unaosimamiwa na Serikali ya CCM kutoa Milioni 600 na kufanya jumla ya Milioni 900 kwa wajasiriamali wanawake Zaidi ya 600 wa Wilaya ya Kinondoni. 

Ndugu Polepole ametoa maelekezo hayo wakati akifungua mafunzo ya Ujasiriamali kwa wanawake wajasiriamali kutoka kata zote za Wilaya ya Kinondoni ambayo yameandaliwa na Madiwani Wanawake wa CCM katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni. 

Akitoa maelekezo mahususi Ndugu Polepole amesema mara baada ya mafunzo hayo kukamilika wakinamama walioshiriki wafanyiwe zoezi la kuhakiki mahitaji ya biashara zao na kwa mujibu wa mahitaji yao halisi ya kukuza mitaji wapewe mikopo hiyo mara moja. 

Aidha Ndugu Polepole amesisitiza kwamba mikopo itakayotolewa na Halmashauri haitakuwa na riba wakati wa marejesho na mikopo itakayotolewa na mfuko wa kujitegemea itakuwa na riba ya asilimia 1.5 kiwango ambacho hakipo katika mabenki ya biashara.

Katika Mafunzo hayo Ndg. Polepole ametumia pia fursa hiyo kueleza na kufafanua kwa ufupi juu ya dhana na uhalisia unaopotoshwa wa Maendeleo ya Vitu na Maendeleo ya Watu na kueleza uhusiano uliokuwepo baina ya maendeleo ya vitu yanavyochochea maendeleo ya watu.

"huwezi kuleta maendeleo ya watu kama hujaweka msingi mzuri wa maendeleo ya vitu,  Serikali ya CCM inajenga barabara kwenda mpaka vijijini ili magari yafike kusafirisha  watu na mazao ya wakulima kitendo ambacho kitapelekea mazao kufika sokoni kwa uhakika na kwa wakati, mazao yakifika sokoni na tukasimama bei kwa haki wakulima watauza kwa faida na tija, watapata pesa na baadae kujikimu mahitaji yao ya kila siku, hayo ndio maendeleo ya watu" Alieleza Ndg Polepole. 

Ndg Polepole ameendelea kwa kusisitiza kuwa, Leo CCM inatoa mafunzo ya ujasiriamali kwa wanawake, na kuweka mindombinu bora ya kupatiwa mikopo, hayo ni maendeleo ya vitu, baadae akinamama hawa watapata mikopo na kufanya biashara ambazo zitawaongezea kipato kitakachowawezesha kumudu mahitaji yao, haya ndiyo maendeleo ya watu. Hivyo ni vema watu wakafahamu maendeleo ya vitu na kwa dnamna yanavyosimamiwa vizuri na CCM yanapelekea kwa haraka maendeleo ya watu.

Ndg Polepole amewataka viongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kuhakikisha wanawapatia mikopo akina mama hao ya jumla ya shilingi milioni 300 kwani zilitengwa kwa ajili hiyo. Aidha, amekemea vikali vitendo vya akinamama kupatiwa mafunzo kisha kuachwa bila kupewa mikopo akikumbusha kuwa serikali ya CCM katika awamu ya tano chini ya Ndg. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM inataka kuona vitendo sio maneno matupu. 

Baadhi ya viongozi waliohudhuria mafunzo hayo ni pamoja Ndg. Harold Maruma Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kinondoni, Bi. Nuru Jackob Katibu wa Umoja wa Wanawake wa Wilaya ya Kinondoni, Madiwani wa Viti Maalumu wa CCM na Ndg. Kazi Maduhu Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (2015-2020). Ambapo CCM imeahidi kuwawezesha wananchi kiuchumi ikiwemo kuwapatia mikopo ya masharti nafuu akinamama, vijana na watu wenye ulemavu.

Imetolewa na,

IDARA YA ITIKADI NA UENEZI
CHAMA CHA MAPINZUZI (CCM)

Maoni